• elisheshe@yahoo.com
  • +255765837485
  • 07 Mar, 2024
  • Admin

SHUKRANI ZETU KWA BWANA PASAKA 2024

Neno la Mungu linatutaka kuwa watu wa shukrani, kwa Bwana Mungu wetu siku zote za maisha yetu. Imetupasa kuwa kila ifikapo majira ya Pasaka wote tutoe shukrani zetu kwa Mungu  tukimshukuru Mungu kwa ndimi za kelele za furaha zilizojaa kicheko kwa kuwa Bwana ametutendea  mambo makuu.Kila mtu katika familia yake kuna mambo makuu Mungu aliyomtendea.Kama familia moja ya Mungu tumshukuru Mungu  kwa mafanikio makubwa yaliopatikana katika elimu.Neno la Mungu katika Mithali 4:13 linatutaka  tumkamate sana elimu,tusimwache aende zake ,tumshike,maana yeye ni uzima wetu.Elimu ni ufunguo wa maisha.

 Mafanikio haya ni ushuhuda wetu kuwa Mungu ametutendea mambo makuu. Kila mtu aandae sadaka yake kwa BWANA na aitoe katika madhabahu ya BWANA.  Neno la kusimamia sadaka zetu Zab 9:1-2 “Nitamshukuru BWANA kwa moyo wangu wote.Nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu.Nitafurahi na kukushangilia  WEWE .Nitaliimbia jina lako wewe uliye juu”.Shukran zinatupa ukaribu na Mungu kila siku. Wimbo: 309 Karibu na wewe Mungu wangu.

Elimu ya Ufalme wa Mungu.

Pamoja na elimu hii ya ulimwengu huu tunatakiwa kuwa na elimu ya ufalme wa mbinguni.Bwana Yesu akawaambia kwa sababu hiyo,Kila mwandishi mwenye elimu ya ufalme wa mbinguni  amefanana na mtu mwenye nyumba  atoaye katika hazina yake  vitu vipya na vya kale (Mathayo 13:52).Elimu ya ufalme wa mbinguni ipitayo elimu zote  tunaipata katika  neno lake takatifu.Bwana wetu Yesu Kristo anataka tujifunze  kwake .Mathayo 11:29 “Jitieni nira yangu mjifunze kwangu ,kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu  wa moyo,nanyi mtapata raha nafsini mwenu.” Mtume Paulo akamwambia Timotheo afanye bidii katika kusoma  na kuonya na kufundisha(Timotheo 4:13) Ndugu zangu tusiwe wavivu wa kusoma  na kujifunza neno la Mungu ili tusije kutupwa huko na huko  na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu  za udanganyifu.Mungu atubariki sisi sote na zaidi sana alibariki neno lake. 

Share This