• elisheshe@yahoo.com
  • +255765837485
  • 13 Oct, 2023
  • Admin


Katika sehemu hii ya pili ya somo letu tutatafakari juu ya nguvu ya uponyaji inayopatikana katika Yesu Kristo Bwana wetu.

            Nguvu hizi za uponyaji zinapatikana katika; neno lake, mwili wake, jina lake na damu yake. Tuanza kwa kuangalia nguvu zilizoko kwenye neno lake. Yesu Kristo ni Neno naye Neno alikuwa Mungu.Yohana 1:1-3 “ Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu.Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. Vyote vilifanyika kwa huyo, wala pasipo yeye hakikufanyika chochote kilichofanyika. “Yesu Kristo ni Neno naye Neno alifanyika mwili akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba , amejaa neema na kweli (Yohana 1:14).Neema na kweli iliyojaa ndani yake ina nguvu ya uponyaji , kwa neno lake Yesu Kristo wagonjwa wakaponywa , viwete wakatembea, wakoma wakatakasika, vipofu wakaona, viziwi wakasikia, vilema wakatiwa nguvu, pepo wakatolewa na bahari ikanyamazishwa kwa ajili ya utukufu wa jina lake. Tutafakari matukio machache ya watu walioponywa na Bwana Yesu kwa kutumia Neno tu bila hata ya kuwagusa. Akida aliyekuwa na mtumishi wake mgonjwa alimwambia Bwana Yesu sema neno tu, na mtumishi wangu atapona. Naye Yesu akamwambia yule Akida.Nenda zako na iwe kwako kama ulivyoamini. Mtumishi wake akapona saa ile ile (Mathayo 8:5-13).Katika kisa cha mama aliyekuwa na binti yake mgonjwa Yesu akamwambia yule mama na iwe kama utakavyo na binti yake akapona tangu saa ile. Kwa neno lake lenye nguvu ya uponyaji aliwatoa pepo, na kuwaponya wote waliokuwa hawawezi. Katika nchi ya Wagerasi watu wawili wenye pepo walikutana naye, wakatoka makaburini, wakali mno, hata mtu asiweze kuipitia ile njia. Yesu aliwatoa pepo hawa kwa neno mmoja tu, Nendeni nao wakatoka wakaingia nguruwe (Mathayo 8:28-32). Wakoma nao walipata nafasi ya kukutana na Bwana Yesu wakatakasika Luka 17:11-15 Yesu alipokuwa akipita katika kijiji kimoja katikati ya Samaria na Galilaya alikutana na watu kumi wenye ukoma; wakasimama mbali, wakapaza sauti wakisema, Ee Yesu, Bwana mkubwa uturehemu. Alipowaona aliwaambia Enendeni, mkajionyeshe kwa makuhani. Ikawa walipokuwa wakienda walitakasika.Vipofu nao walimwendea Yesu ili wapate kuona , kwa neno lake tu walipata kuona Marko 10:46-52 .Huko Yeriko kulikuwa na kipofu mmoja alikuwa ameketi kando ya njia, aliposikia Yesu anapita akapaza sauti yake na kusema, Mwana wa Daudi Yesu unirehemu.Yesu akamjibu akamwambia wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia Mwalimu wangu, nataka nipate kuona .Yesu akamwambia , enenda zako, imani yako imekuponya mara akapata kuona , akamfuata njiani .Sehemu nyingine inayotuonyesha nguvu ya uponyaji iliyoko katika neno lake ni pale alipokutana na watu waliopooza. Mathayo 9:1-8. Wakamletea mtu mwenye kupooza, amelala kitandani; naye Yesu alipoona imani yao, alimwambia yule mwenye kupooza, jipe moyo mkuu, mwanangu, umesamehewa dhambi zako. Ondoka ujitwike kitanda chako, uende nyumbani kwako. Akaondoka akaenda zake nyumbani kwake. Marko 3:1-5. Akaingia tena katika sinagogi, na palikuwepo mtu mwenye mkono uliopooza na ilikuwa siku ya sabato.Akamwambia yule mtu nyosha mkono wako, naye akaunyosha, mkono wake ukawa mzima tena .Neno la Yesu lina nguvu sana hata upepo wa bahari humtii. Mathayo 8:23-27 na Marko 4:35-41 wanaelezea kisa cha Bwana Yesu na wanafunzi wake wakiwa chomboni baharini. Ikatokea dhoruba kuu ya upepo , mawimbi yakapiga chombo hata kikaanza kujaa maji wakati huo Yesu amelala wanafunzi wake wakamwendea wakamwamsha, wakisema, Bwana tuokoe, tunaangamia.Akawaambia mbona mmekuwa waoga , enyi wa imani haba hamna imani bado. Akaamka akaukemea upepo, akaiambia bahari, nyamaza utulie.Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu. Huyu ndiye Yesu Kristo ambaye hata pepo na bahari zamtii.Katika somo hili tumeona jinsi Bwana Yesu kwa kutumia neno lake tu alivyoweza kuwaponya vilema, viwete, vipofu na wakoma.Kwa njia hii ya miujiza watu waliuona utukufu wa Mungu na Mwanae hata wengine wakamtukuza Mungu wakisema hakika huyu ni Mwana wa Mungu.

Katika sehemu hii inayofuata tutatafakari nguvu za uponyaji zilizoko ndani ya mwili wake na kwenye mkono wake. Mathayo 26:26 “Nao walipokuwa wakila Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake akasema twaeni mle huu ndio mwili wangu.” Mwili wa Yesu ni chakula cha uzima cha kiroho na kimwili. Waulao mwili wa Kristo kwa imani wana uzima ule wa milele na hao ni wale wanaotambua kwamba mkono wa kuume wa BWANA hutenda makuu na tena mkono wa kuume wa BWANA umetukuzwa .Tuangalie matukio machache yanayoonyesha nguvu ya uponyaji iliyoko katika mwili wa Yesu na katika mikono yake. Marko 5:25-32. Habari hii ni ya mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili aliyegusa vazi la Yesu, maana alisema nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona.Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule.Mara Yesu , hali akifahamu nafsini mwake kwamba nguvu zimemtoka, akageuka akasema, ni nani aliyenigusa mavazi yangu.Wanafunzi wake kwa kutokujua kuwa mguso ule ulikuwa na imani ndani yake wakafikiri ameguswa kutokana na msongamano wa watu, lakini Bwana Yesu anayetambua roho na nafsi zetu aliiona imani ya yule mwanamke.Akatazama pande zote ili amwone yule aliyetenda neno hilo. Na yule mwanamke akaingiwa na hofu na kutetemeka akijua lililompata, akaja akamwangukia, akamweleza kweli yote. Akamwambia, binti , imani yako imekuponya enenda zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena.Hapa tunaona mguso uliotoa nguvu za uponyaji ndani ya mwili wa Bwana Yesu.Je, wewe, uko tayari kumgusa Bwana Yesu upate amani na uponyaji wa kimwili na kiroho? Mtu mwingine ambaye Yesu alimgusa akapona ni mkwe wa mtume Petro.Mathayo 8:14-15 .” Hata Yesu alipofika nyumbani kwa Petro , akamwona mkwe wa Petro, mamaye mkewe, amelala kitandani hawezi homa. Akamgusa mkono, homa ikamwacha, naye akaondoka akawatumikia.Katika nchi ya Genesareti walipomtambua walituma watu kwenda nchi zile zilizo kando kando wakamletea wote waliokuwa hawawezi ; nao wakamsihi waguse hata pindo la vazi lake tu, na wote waliogusa wakaponywa kabisa (Mathayo 14:34-36). Mathayo 9:27-29 “Yesu alipokuwa akipita kutoka huko, vipofu wawili wakamfuata wakipaza sauti wakisema, uturehemu Mwana wa Daudi. Naye alipofika nyumbani wale vipofu walimwendea Yesu akawaambia; Mnaamini kwamba naweza kufanya hili? Wakamwambia Naam, Bwana. Ndipo alipowagusa macho, akasema kwa kadiri ya imani yenu mpate. Macho yao yakafumbuka”.Marko 3:10 “ Maana aliponya wengi hata wote waliokuwa na msiba wakamrukia wapate kumgusa.” Nguvu zingine za uponyaji tunazishuhudia katika mkono wake. Kila mwenye imani Bwana Yesu alipomgusa kwa mkono wake au kumshika mkono alipata uzima au uponyaji.

  • Marko 1:40-42 “ Akaje kwake mtu mwenye ukoma , akamsihi na kumpigia magoti na kumwambia, ukitaka ,waweza kunitakasa .Naye akamhurumia, akanyosha mkono wake akamgusa akamwambia, nataka takasika.Na mara ukoma wake ukamtoka akatakasika.
  • Marko 5:22-23 , 41 “ Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi , jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguu pake , akimsihi sana akisema, binti yangu mdogo yu katika kufa, nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona na kuishi.Akaingia ndani alimokuwepo yule kijana , akamshika mkono kijana akamwambia, Talitha, kumi, tafsiri yake, msichana nakuambia, inuka .Mara akasimama yule kijana akaenda zake.” Hapa tunaona kijana aliyekufa ambaye Bwana Yesu anasema amelala tu akiinuliwa kwa kushikwa mkono naye akapata uzima .
  • Marko 6:5-6 “ Wala hakuweza kufanya muujiza wowote huko (nchi ya kwao), isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache , akawaponya”
  • Marko 7:32-35 “ Wakamletea kiziwi, naye ni mwenye utasi wakamsihi amwekee mikono .Akamtenga na mkutano faraghani, akatia vidole vyake masikioni mwake, akatema mate, akamgusa ulimi, akatazama juu mbinguni, akaugua, akamwambia Efatha, maana yake, Funguka. Mara masikio yake yakafunguka , kifungo cha ulimi wake kikalegea akasema vizuri”.
  • Marko 8:22-25 “Wakafika Bethsaida, wakamletea kipofu wakamsihi amguse.Akamshika mkono yule kipofu, akamchukua nje ya kijiji, akamtemea mate ya macho, akamwekea mikono yake, akamwuliza, waona kitu? Akatazama juu akasema naona watu kama miti, inakwenda.Ndipo akaweka tena mikono yake juu ya macho yake , naye akatazama sana; akawa mzima , akaona vyote waziwazi.
  • Yohana Mtakatifu 9:1-7 Habari hii ni mtu kipofu tangu kuzaliwa .Bwana Yesu anasema huyu hakutenda dhambi wala wazazi wake, bali kazi za Mungu zidhihirishwe ndani yake.Alipokwisha kusema hayo, alitema mate chini, akafanya tope kwa yale mate. Akampaka kipofu tope za macho, akamwambia , nenda kanawe katika birika ya Siloamu, (maana yake , aliyetumwa). Basi akaenda na kunawa; akarudi anaona .Je, ndugu yangu mpendwa uko tayari kushikwa mkono na Bwana Yesu? Na kuwaleta wengine kwa Bwana Yesu ili wapate uponyaji na uzima wa milele? Tusema kama huyu kipofu alipoulizwa wasemaje katika habari zake huyu aliyekufumbua macho? Akasema , Ni nabii . Nami nasema kwa ujasiri kuwa huyu ni yule nabii, Yesu wa Nazareti ya Galilaya .

Jina la Yesu Kristo wa Nazareti ya Galilaya lina mamlaka, uweza na nguvu kubwa ya uponyaji, hili ni jina lipitalo majina yote hapa duniani , kule mbinguni na hata kule kuzimu. Wafilipi 2:9-11 “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno,akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe , la vitu vya mbinguni na vya duniani, na vya chini ya nchi, na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.” Yesu Kristo ametupa jina hili lenye nguvu ili na sisi watumishi wake tuweze kuendeleza ufalme wa Mungu.Kwa njia hii Mungu anafanya miujiza hata leo kupitia watumishi wake wapakwa mafuta wa Bwana. Matendo ya miujiza na uponyaji ni karama ambazo anatoa Roho Mtakatifu kwa wote wamwaminio. Wakolosai 3:17 “ Na kila mfanyalo kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.” Tumshukuru Mungu Baba siku zote kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Kristo, hali tukinyenyekea katika kicho cha Kristo.

Ni jambo la kweli na hakika kwamba Jina la Yesu linayo nguvu ya kumsaidia mtu aaminiye kufanya jambo lolote hapa duniani, mradi tu liwe ni jambo jema la kumpendeza Mungu.

Katika somo hili tutatafakari zaidi nguvu za jina la Yesu katika miujiza ya uponyaji wa kimwili na kiroho.Mathayo 10:1-8 “Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina.” Katika Marko 16:15-17 Bwana Yesu anatoa amri kwa wanafunzi wake,”Akawaambia enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka, asiyeamini atahukumiwa.Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio, kwa jina langu watatoa pepo, watasema kwa lugha mpya, watashika nyoka, hata wakinywa kitu cha kufisha hakitawadhuru kabisa, wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.” Hakika yote yanawezekana kwake yeye aaminiye.Na hii ndiyo amri yake, kwamba tuliamini jina la Mwana wake Yesu Kristo, na kupendana sisi kwa sisi, kama alivyotupa amri (amri hii nawapa pendaneni). Yohana 3:18”Amwaminiye yeye hahukumiwi, asiyemwamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.” Yesu Kristo katika Yohana 14:12-14 anasema, “ Amini , amin, nawaambieni, yeye aniaminiye mimi,kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya, naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.” Yesu Kristo anasema tukimwomba baba neno lolote atatupa kwa jina lake.Hata sasa tukiomba neno kwa jina lake tutapata ili furaha yetu iwekamilifu kila atakayeliitia jina la Bwana ataokolewa.Wanafunzi wa Bwanaa Yesu walitoka wakahubiri kote kote. Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo.Mungu akafanya miujiza ya kupita kawaida kwa mikono ya Paulo Mtume. Matendo 19:11-12.” Mungu akafanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida, hata wagonjwa wakaletewa leso na nguo zilizotoka mwilini mwake, magonjwa yao yakawaondokea, pepo wachafu wakawatoka”. Paulo alimponya baba yake Publio aliyekuwa anaumwa homa na kuhara damu.Matendo 28:8-9 “Ikawa babaake Publio alikuwa hawezi homa na kuhara damu Paulo akaingia kwake akaomba, akaweka mikono yake juu yake, na kumpoza. Yalipokwisha kutendeka hayo wengine waliokuwa na wagonjwa katika kisiwa wakaja wakapozwa.” Kando ya magonjwa hata pepo wanatii jina la Yesu Kristo.Luka 10:17-20 2 Ndipo wale sabini waliporudi kwa furaha wakisema, Bwana hata pepo wanatutii kwa jina lako.” Yesu akawaambia msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii, bali furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni. Akatokea mtu mmoja ambaye hakuwa pamoja na wanafunzi lakini aliweza kutoa pepo. Marko Mtakatifu 9:38-40 “Yohana akajibu, akamwambia, Mwalimu, tulimwona mtu akitoa pepo kwa jina lako, ambaye hafuatani nasi; tukamkataza, kwa sababu hafuatani nasi. Yesu akasema, msimkataza kwa kuwa hakuna mtu atakayefanya muujiza kwa jina langu akaweza mara kuninenea mabaya, kwa sababu asiye kinyume chetu, yu upande wetu.” Walitokea watu wengine ambao hawako upande wa Bwana Yesu nao wakajaribu kutoa pepo kwa jina la Yesu.Yule pepo akawaambia tunamjua Paulo na tunamjua Yesu ninyi ni nani? Kwa hasira wale pepo wakawarukia na kuwashinda nguvu nao wakakimbia kwa hofu.Jina hili linatumika kwa wale waaminio kuwa Yesu ni Bwana na mwokozi wa maisha yao (waliookoka). Paulo alimponya kijakazi mmoja aliyekuwa na pepo wa uaguzi. Matendo ya Mitume 16:16-18 “Ikawa tulipokuwa tukienda mahali pale pa kusali, kijakazi mmoja aliyekuwa na pepo wa uaguzi akatukuta, aliyewapatia bwana zake faida nyingi kwa kuagua.Akamfuata Paulo na sisi akipiga kelele, akisema, watu hawa ni watumishi wa Mungu aliye juu, wenye kuhubiri njia ya wokovu .Akafanya hayo siku nyingi. Lakini Paulo akasikitika , akageuka akamwambia yule pepo, nakuamuru kwa jina la Yesu Kristo mtoke huyu. Akamtoka saa ile ile.” Jina la Yesu lina nguvu nyingi linaponya viwete. Matendo 3:1-10 Petro na Yohana walikuwa wakikwea pamoja kwenda hekaluni, saa ya kusali saa tisa. Na mtu mmoja aliyekuwa kiwete toka tumboni mwa mamaye alichukuliwa na watu na kuwekwa kwenye mlango wa hekalu uitwao Mzuri.Alipowaona Petro na Yohana aliwaomba sadaka .Lakini Petro akasema , mimi sina fedha , wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti; simama uende. Akaondoka upesi akasimama, akaanza kwenda akiruka-ruka kwa furaha na kumsifu Mungu.Katika Waraka wa Yakobo 5:14-16 neno la Mungu linatufundisha kuwa jina la Yesu linaweza kutumika pamoja na mafuta kumpaka mgonjwa naye akapona. “Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa Kanisa , nao wamwombea na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua, hata ikiwa amefanya dhambi atamsamehe .Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana mpate kuponywa”. Katika matendo haya makuu aliyoyafanya Bwana Yesu na wanafunzi wake yalifanyika ili Mungu asifiwe na kutukuzwa. Walioponywa walimtukuza Mungu na wale walioshuhudia matendo hayo walimsifu na kumtukuza Mungu .Matendo 19:17-18, 20 “Habari hii ikajulikana na Wayahudi wote na Wayunani waliokaa Efeso, hofu ikawaingia wote, na jina la Bwana Yesu likatukuzwa. Na wengi   wa wale walioamini wakaja wakaungama , wakidhihirisha matendo yao.Hivyo ndivyo neno la Bwana lilizidi na kushinda kwa nguvu .Bwana akalizidisha kanisa kila siku kwa wale waliokuwa wakiokolewa.

Sehemu hii ya mwisho ya somo hili tutatafakari nguvu iliyoko ndani ya damu ya Yesu.Ni damu yenye nguvu ipitayo damu ya mafahali. Katika Agano la Kale damu ya mafahalli (ng’ombe na kondoo) ilitumika kama sadaka ya ondoleo la dhambi . Waebrania 9:22 “Na katika Torati karibu vitu vyote husafishwa kwa damu na pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo.” Katika Agano Jipya Mungu Baba amemtoa mwanawe wa pekee Yesu Kristo kuwa Mwana –kondoo wa sadaka kwa ajili ya ondoleo la dhambi zetu sisi wanadamu . Huyu ndiye Yohana Mbatizaji alipomwona alisema, “ Ndiye yule ajaye nyuma yangu, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya kiatu chake.Siku ya pili yake amwona Yesu anakuja kwake akasema , Tazama, Mwana- kondoo wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu (Yohana 1:27,29).” Huyu ndiye Yesu Kristo aliyesulubiwa pale msalabani Golgota na damu yake ya agano jipya ikamwagika.

Hii ndiyo damu ambayo tutatafakari nguvu zake za uponyaji wa kimwili na kiroho. Damu ya Yesu ina nguvu ya kukuondolea shida zako zote ikiwa una imani, unapotamka damu ya Yesu katika maisha yako unatakiwa uwe na imani ya kutosha juu ya nguvu na uwezo wa hiyo damu hapo ndipo utaona matendo makuu ya Mungu kama vile uponyaji. Hakika ipo nguvu ya ajabu ndani ya damu ya Yesu. Kwa njia ya imani katika damu yake, damu ya Yesu inafanya mambo mengi sana; inatakasa ulimwengu, inaponya na kutulinda, inanena mema juu yetu, inamshinda shetani, inaleta ondoleo la dhambi, na kufanya upatanisho baina ya Mungu na wanadamu inatupa uzima wa milele, haina mwisho wala haipungui nguvu.

  • Damu ya Yesu inatakasa. Waebrania 10:14 “Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa.” Waebrania 13:12 “Kwa ajili hii Yesu naye, ili awatakase watu kwa damu yake mwenyewe, aliteswa nje ya lango.” Basi tutoke tumwendee maana hapa hatuna mji udumuo, bali twautafuta ule ujao.
  • Damu ya Yesu inaponya na kutulinda. 1Wakorintho 15:57 “Lakini Mungu ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo,” Pia katika Ufunuo 12:11 anasema, “Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana –kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa.” Hawa ni wale waliofua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-kondoo.Ufunuo 7:16-17 “Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena, wala jua halitawapiga, wala hari iliyo yote kwa maana huyo Mwana – kondoo, aliyeketi katika kiti cha enzi atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchem za maji yenye uhai, na Mungu atafuta machozi yote katika macho yao”.Lakini katika mambo hayo yote tunashinda na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda (yaani Yesu Kristo).
  • Damu ya Yesu inanena mema.Waebrania 12:24 “Na Yesu mjumbe wa agano jipya na damu ya kunyunyiziwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili.” Damu ya Yesu inanena mema katika maisha yetu yote, maisha ya kuwa na afya njema, ujasiri na ukombozi .Waebrania 10:19 “ Basi ndugu , kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu.” Waebrania 9 :12-14 “ Wala si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele”. Damu ya Yesu inatunenea mema wala si mabaya, inatusafisha dhamira zetu na matendo mafu, tupate kumwabudu Mungu aliye hai katika kweli yote.
  • Damu ya Yesu inaleta ondoleo la dhambi. Mathayo 26:27-28“Akakitwaa kikombe, akashukuru akawapa akisema, nyweni nyote katika hiki, kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi”. Katika Wakorintho 11:25 neno la Mungu linasema, “Na vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe akisema, kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, fanyeni hivi kila mnywapo kwa ukumbusho wangu.” Huyo manabii wote humshuhudia ya kwamba kwa jina lake amwaminiye atapata ondoleo la dhambi.Ondoleo la dhambi linapatikana kwa njia ya TOBA.Waefeso 1:7 2 “Katika yeye huyo, kwa damu yake, tunao ukombozi wetu, msasamaha ya dhambi, sawasawa na wingi wa neema yake.” Dhambi zetu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyepe kama theluji, zijapokuwa nyekundu kama bendera zitakuwa kama sufu.Yesu Kristo ni shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa na mkuu wa wafalme wa dunia .Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake (Ufunuo 1:5).Katika Waraka wa kwanza wa Yohana 1:7 “Bali tukienenda Nuruni, twashirikiana sisi kwa sisi na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote .” Katika damu ya Yesu tunahesabiwa haki na tunaokolewa na ghadhabu kwa yeye. Waebrania 13:20-21 “ Basi , Mungu wa amani aliyemleta tena kutoka kwa wafu Mchungaji mkuu wa kondoo, kwa damu ya agano la milele, yeye Bwana wetu Yesu awafanye ninyi kuwa wakamilifu katika kila tendo jema, mpate kuyafanya mapenzi yake, naye akifanya ndani yetu lipendezalo mbele zake, kwa Yesu Kristo, utukufu unaye yeye milele na milele Amina.”
  • Damu ya Yesu inatupatanisha na Mungu: Tunahitaji tupatanishwe na Mungu kwa kuwa dhambi imetutenga na uso wa Mungu.Isaya 59:2 2 “Lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mugu wenu na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone , hata hataki kusikia.” Dhambi hututenganisha na Mungu na utukufu wake kiasi kwamba hasikii maombi yetu.Mshahara wa dhambi ni mauti na kutengana na Mungu milele .Tunapoteza haki yetu ya kuitwa wana wa Mungu au watoto wa Mungu .Tunapata haki ya kupatana na Mungu wetu kwa neema yake kupitia damu ya Yesu.Tumehesabiwa haki bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu, ambaye Mungu amekwisha kumweka awe upatanisho kwa njia ya imani katika damu yake (Warumi 3:24-25).Wakolosai 1:19-20 “ Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake, kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi au vilivyo mbinguni.” Ni kweli kwamba Mungu ndiye aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo ambaye alitupa huduma ya upatanisho .2 Wakorintho 5:19 “ yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao, naye ametia ndani yetu neno la upatanisho .”Tukishapatanishwa na Mungu tunapata neema na amani ya Mungu. Damu ya Yesu inatupatanisha na Mungu tunapotubu dhambi zetu na kumrudia yeye .Neno la Mungu lilimjia nabii Yeremia kwa ajili ya Israeli na nyumba ya Yuda na juu ya mataifa yote likisema, (Isaya (36:3) “Huenda nyumba ya Yuda watasikia mabaya yote niliyokusudia kuwatenda, wapate kurudi, kila mtu akaiache njia yake mbaya, nami nikawasamehe uovu wao na dhambi yao.” Tukitubu dhambi zetu na kumrudia Mungu anatusamehe na kutupatanisha naye kwa damu ya Yesu.Mungu anatutaka na sisi tuwe wapatanishi kama alivyo yeye. Mathayo 5:9 “Heri wapatanishi, maana hao wataitwa wana wa Mungu.” Tunatakiwa tupatane na ndugu yaani sisi kwa sisi na tuwapatanishe watu na Mungu kwa kuwafundisha neno lake. Neno la Mungu linatuagiza kuwa hata ukiwa na sadaka yako mkononi uiache madhabahuni ukapatane kwanza na ndugu yako ndio uje uitoe Mathayo 5:23). Marko 11:25-26 “ Nanyi kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neo juu ya mtu , ili Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu .Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.” Mungu ni mpatanishi na ameweka nguvu kubwa katika neno hili la upatanisho na kusamehe kwa hiyo kila tuombapo upatanisho lazima tuitie damu ya Yesu kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Kristo Yesu, ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote.
  • Damu ya Yesu inatupa uzima wa milele. Yohana 6:53-59 “ Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake.Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi , nami ni hai kwa Baba , kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi.Hiki ndicho chakula kishukacho kutoka mbinguni si kama mababa walivyokula wakafa, bali akilaye chakula hicho ataishi milele.Maneno hayo aliyasema (Bwana Yesu) katika sinagogi , alipokuwa akifundisha huko Kapernaumu.” Lakini kuna wengine ambao hawakuamini maneno hayo, wakarejea nyuma , wasiandamane naye tena. Basi Yesu akawaambia wale Thenashara, Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka? Basi Simon Petro akamjibu , Bwana twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.Tunajifunza kutokana na jibu la Simon Petro kuwa neno la Mungu lina uzima wa milele.Yohana 3:16” Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele”. Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa, ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele tena awe nao tele .Hatuna budi kuwa na ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu, Baada ya mioyo yetu kunyunyiziwa damu ya Yesu na kuacha dhamira mbaya. Waraka kwa Waebrania 9:12-15 “Wala si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele. Kwa maana, ikiwa damu ya mbuzi na mafahali na majivu ya ndama ya ngo’mbe waliyonyunyiziwa wenye uchafu hutakasa hata kuusafisha mwili; basi si zaidi damu yake Kristo ambaye kwamba kwa Roho wa milele alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa, itawasafisha dhamira zenu na matendo mafu, mpate kumwabudu Mungu aliye hai. Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya, ili mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele”. Neno la Mungu linasema kwamba tunahesabiwa haki katika damu ya Yesu, tutaokolewa na ghadhabu ya Mungu. Warumi 1:18 “Kwa maana ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote na uovu wa wanadammu waipingao kweli kwa uovu”. Wale ambao wanamwamini mwana na wenye saburi katika kutenda mema wanatafuta utukufu na heshima na kutokuharibika, watapewa uzima wa milele, na wale wenye fitina, wasiotii kweli, bali wakubalio dhuluma, watapata hasira na ghadhabu (Warumi 2:7-8).Katika kitabu cha Yohana 3:36 neno la Mungu linasema, “ Amwiniye Mwana yuna uzima wa milele, asiyemwamini mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inamkalia.” Waraka wa kwanza wa Yohana 5:11-12 “Na huu ndio ushuhuda ya kwamba alitupa uzima wa milele; na uzima huu umo katika Mwanae.Yeye aliye naye, mwana anao huo uzima, asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima.” Mtu ambaye ameula mwili wa Kristo na kuinywa damu yake iliyomwagika pale msalabani ni yule ambaye anakaa ndani ya mwana, na ndani ya Baba. Na hii ndiyo ahadi aliyotuahidia yaani uzima wa milele. Unapompokea Yesu Kristo moyoni mwako unapokea uzima wa milele kwa kuwa ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu (Yohana 1:4). Tunapompokea Yesu Kristo kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yetu na kukaa ndnai yake tunapata heshima ya kuitwa wana wa Mungu au watoto wa Mungu , tunakuwa viumbe wapya .2 Wakoritho 5:17 “ Hata imekuwa mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya, ya kale yamepita tazama yamekuwa mapya.” Hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu kwa kuwa Kristo ameyafanya yote kuwa mapya.                

Share This